Thursday, October 31, 2013

Saini zakusanywa kumng’oa Makinda



Dodoma. Mbunge wa Nzega, Dk Khamis Kigwangalla, (CCM), leo anatarajiwa kuanza kukusanya saini za wabunge akitafuta kuungwa mkono katika hoja ya kutokuwa na imani na Spika wa Bunge, Anne Makinda kwa madai kwamba amekuwa akikiuka kanuni za Bunge.

Dk Kigwangalla aliibua hoja ya kutokuwa na imani na Spika katika kikao cha wabunge wote cha kuelezea shughuli zitakazofanywa na Bunge katika mkutano wa 13, kilichofanyika juzi jioni kwenye ukumbi wa Pius Msekwa.

Mbunge huyo ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, jana alithibitisha kuwapo kwa mjadala huo katika kikao cha wabunge, lakini hakuwa tayari kueleza kwa undani na badala yake alisema kwamba leo ataanza kukusanya saini za wabunge kwa ajili ya kukamilisha hoja ya kutokuwa na imani na Spika Makinda.

Chanzo chetu kutoka katika kikao hicho cha wabunge kilibainisha kuwa Kigwangalla alihoji kuhusiana na Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Bajeti, Andrew Chenge (CCM-Bariadi Magharibi) kuteuliwa na Spika wakati katika kamati nyingine wenyeviti na makamu huchaguliwa na wajumbe wa kamati husika.

Pia Dk Kigwangala alisema Spika Makinda alivunja kanuni kwa kuwapa posho ya Sh430,000 kwa siku wajumbe wa kamati inayoongozwa na Chenge wakati wajumbe wa kamati nyingine wamekuwa wakipewa Sh130,000.

“Anachokifanya Spika ni matumizi mabaya ya fedha za umma, inakuwaje wengine wafanye kazi hata bila posho lakini wao (Kamati ya Bajeti), walipwe posho ya Sh430,000 kwa siku?” chanzo hicho kilimkariri Dk Kigwangalla akihoji. Hata hivyo, Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashililah akizungumza na gazeti hili jana alisema mazingira ya kamati fulani kupata malipo ya ziada tofauti na viwango vya kawaida hutokea pale uongozi wa kamati husika unapoomba kwa Spika.

“Si kweli kwamba Kamati ya Bajeti inalipwa fedha za ziada kila wakati, hapana, ni pale tu wanapoomba malipo hayo kutokana na sababu ambazo lazima Spika aridhike nazo. Ieleweke kuwa siyo kamati hiyo tu, kwa sasa Kamati ya Katiba, Sheria na Utawala ambayo inachambua miswada mingi nayo imekuwa ikiomba na baada ya Spika kuridhia basi nao wanapewa,” alisema Dk Kashililah.

Katibu huyo wa Bunge alieleza kuwa zaidi ya kamati nane zimewahi kuomba malipo ya ziada kwa maana ya kutaka posho zaidi, ulinzi, usafiri na hata chakula, ikiwa zinakabiliwa na majukumu ya ziada pia katika mazingira tofauti nje ya utaratibu wa kawaida.

“Kimsingi, kamati nyingi zinapewa malipo tofauti, watu wanaweza kuwa na kazi mpaka saa saba au nane usiku, au wanakwenda kufanya kazi katika mazingira yasiyokuwa ya kawaida, taratibu zinamruhusu Spika kama akiridhika na maelezo ya kazi husika, basi anaruhusu kutekelezwa kwa maombi hayo,” alisema Dk Kashililah.

Kuhusu Serukamba

Aidha, Dk Kigwangalla alinukuliwa akisema Spika amekiuka kanuni kwa kumchagua Mwenyekiti wa Kamati ya Miundombinu, Peter Serukamba (Kigoma Mjini-CCM), kuwa mjumbe wa Kamati ya Bunge ya Bajeti.

“Hakuna mbunge yeyote aliyepo katika kamati mbili lakini hata kungekuwa na sababu maalumu basi wa kuteuliwa angekuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Uchumi, Viwanda na Biashara, Mahmoud Mgimwa (Mufindi Kaskazini-CCM) ambaye TRA (Mamlaka ya Mapato Nchini) ipo chini ya kamati yake,” kilisema chanzo hicho.

No comments:

Post a Comment

PLEASE LEAVE YOUR COMMENTS HERE. HELP BLOG DEVELOPMENT

Print It: