Thursday, October 31, 2013

VITA POLISI NA MASHABIKI MSIMBAZI; NI BAADA YA SARE YA 1-1 DHIDI YA KAGERA



UWANJA wa Taifa, Dar es Salaam leo uligeuka eneo la vita baina ya Polisi mashabiki wa Simba SC, kufuatia Kagera Sugar kupata bao la kusawazisha dakika ya pili ya muda wa nyongeza baada ya kutimia kwa dakika 90 za mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, timu hizo zikitoka 1-1.
Baada ya Salum Kanoni kukwamisha nyavuni mkwaju wake wa penalti, mashabiki wa Simba waliokuwa viti vya Rangi ya Bluu na Chungwa, walianza kung’oa viti na kuvitupia uwanjani.


Mara moja, Polisi walianza kupambana na mashabiki hao kwa kuwatupia mabomu ya machozi, ndipo wakaanza kukimbia. Makocha na wachezaji wa Simba kwa pamoja waliwafuata waamuzi kuwalalamikia- hali ambayo ilifanya watolewe kwa kusindikizwa
na Polisi.
Katika mchezo huo, uliochezeshwa na refa Mohamed Theofile wa Morogoro aliyesaidiwa na Said Mnonga na Charles Chambea wote wa Mtwara, ambao walishindwa kuumudu kabisa, hadi mapumziko, Simba SC walikuwa mbele kwa bao 1-0.

Bao hilo lilifungwa na mshambuliaji wa kimataifa wa Burundi, Amisi Tambwe dakika ya 45 baada ya kupokea pasi nzuri ya Betram Mombeki na kumpiga chenga beki Salum Kanoni, kabla ya kumchambua kipa Hannington Kalyesebula.
Kagera ilipata pigo mapema dakika ya 22 kipa wake Agathon Anthony kuumia katika harakati za kuzuia shambulizi la Tambwe na nafasi yake ikachukuliwa na Mganda, Kalyesebula.
Kwa ujumla timu zote zilishambuliana kwa zamu kipindi cha kwanza, ingawa Simba SC ndiyo waliotengeneza nafasi nyingi zaidi za kufunga.
Kipindi cha pili, Simba SC iliendelea kusukuma mashambulizi mengi langoni mwa Kagera, lakini washambuliaji wake walikosa umakini wa kutumia nafasi.
Kagera nayo iliendelea kushambulia na kwa ujumla mchezo ulizidi kunoga kadiri muda ulivyokuwa ukisonga mbele kutokana na ushindani mkali.
Wakati refa wa akiba, Hussein Kalindo wa Kinondoni, amekwishaonyesha dakika nne za nyongeza, Kagera ikafanya shambulizi langoni mwa Simba na Daudi Jummane akaangushwa kwenye eneo la hatari na beki wa Simba SC, Joseph Owino na refa akaamuru penalti.
Beki wa zamani wa Simba SC, Salum Kanoni akaenda kumchambua vizuri kipa Abuu Hashimu kuisawazishia Kagera dakika ya 90+2.
Simba SC; Abuu Hashim, Nassor Masoud ‘Chollo’, Issa Rashid, Joseph Owino, Hassan Khatib, Jonas Mkude, Ramadhani Singano, Said Ndemla, Betram Mwombeki, Amisi Tambwe na William Lucian.

Kagera Sugar; Agathon Anthony/Hannington Kalyesebula dk22, Salum Kanoni, Martin Muganyizi, Ernest Mwalupani, Malegesi Mwangwa, Zuberi Dabi/Juma Mpola dk46, Benjamin Asukile/Adam Kingwande dk46, George Kavilla, Themi Felix, Daudi Jumanne na Paul Ngwai.


IMETOKA THE CHOICE

No comments:

Post a Comment

PLEASE LEAVE YOUR COMMENTS HERE. HELP BLOG DEVELOPMENT

Print It: